Breaking


Ijumaa, 12 Septemba 2025

ZINGATIENI MASLAHI YA WATUMISHI WA UMMA KWENYE MAENEO YENU.


Mkurugenzi wa Idara ya Serikali za Mitaa kutoka Ofisi ya Rais TAMISEMI Bi. Angelista Kihaga amewataka Maafisa Bajeti wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa  kuzingatia na kusimamia maslahi ya Watumishi katika kipindi cha kuandaa Bajeti zao.

“Mipango tunayoipanga tuhakikishe inajumuisha stahiki za watumishi katika ngazi zote kuanzia makao makuu Hadi katika ngazi za msingi” Bi. Kihaga.

Bi. Kihaga ameyasema hayo wakati akifunga mafunzo ya uandaaji na utekelezaji wa Mipango na Bajeti kwa Maafisa Bajeti wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa 2025 yaliyofanyika Jijini Dodoma.

Amesema katika usimamizi wa rasilimali watu ni muhimu Maafisa Bajeti  kuzingatia stahiki za watumishi kama ambazo wamekuwa wakizidai kama vile Malipo ya kwaajili ya likizo na ugonjwa kwa kufuata kanuni na Sheria za Bajeti 

Aidha, Bi kihaga amewataka Maafisa Bajeti kwenda kusimamia kwa ukaribu miradi mbali mbali ya maendeleo inayotekelezwa katika maeneo Yao na kuhakikisha inaendana na thamani ya fedha.

Mafunzo hayo yaliyofanyika kwa siku nane yakifanyika katika makundi manne yamejumuisha Maafisa Bajeti 396 kati Yao  41 ni kutoka katika Tawala za Mikoa na 355 kutoka katika Mamlaka za Serikali za Mitaa.

Hakuna maoni: