Msanii maarufu wa muziki wa injili, Rose Muhando, ameamua kuvunja ukimya baada ya takribani miaka 15 ya kuvumilia maumivu na madai ya kudhulumiwa haki zake za mapato kutokana na kazi zake za muziki zilizo kwenye majukwaa ya kidijitali.
Kupitia ujumbe wake, Rose Muhando amesema kwa muda mrefu amekuwa akiamini haki yake itapatikana bila kulazimika kuzungumza hadharani. Hata hivyo, amesema maumivu aliyopitia yamemlazimu sasa kufungua kinywa na kueleza kilichomsibu.
Kwa mujibu wa maelezo yake, chanzo cha tatizo ni ushirikiano wake wa zamani na kampuni ya Sony, ambao licha ya kusitishwa kitambo, kampuni hiyo bado inashikilia zaidi ya kazi zake 37. Rose anadai kuwa hadi sasa kazi hizo bado hazijaachiliwa kwake, wala hajawahi kupata hata shilingi moja kama mapato, ilhali ni kazi alizozifanyia jasho kwa miaka mingi.
Msanii huyo amesema Serikali kupitia COSOTA Tanzania imejaribu kuingilia kati na kusimamia haki yake, lakini juhudi hizo zimedaiwa kukwama kutokana na kukosekana kwa ushirikiano kutoka kwa mwakilishi wa kampuni husika, aliyemtaja kuwa Bi. Seven Mosha, ambaye anadaiwa kuitwa mara kadhaa bila kutoa ushirikiano wowote.
Rose Muhando amesema hali hiyo siyo tu imemuumiza binafsi, bali pia inakatisha tamaa na kurejesha nyuma ndoto za wasanii wengi wanaodhulumiwa haki zao kimyakimya bila sauti kusikika.
Kwa unyenyekevu, msanii huyo ameandika kwa Serikali, akimuomba moja kwa moja Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mheshimiwa Paul Christian Makonda, kuingilia kati suala hilo kwa haraka ili haki itendeke.
ROSE MUHANDO AMEANDIKA HIVI:
“NI MUDA MREFU SANA UMEPITA TAKRIBANI MIAKA 15 NIMEKUWA NIKINYAMAZA, NIKIVUMILIA KWA MOYO WOTE, NIKIAMINI HAKI YANGU NITAIPATA LAKINI LEO, MAUMIVU YAMENILAZIMU KUFUNGUA MDOMO NA KUSEMA.
KWA MUDA MREFU SASA, NIMEKUWA NIKIDHULUMIWA HAKI YANGU YA MAPATO KUTOKANA NA KAZI ZANGU KATIKA MAJUKWAA YOTE YA KIDIJITALI. HAYA YOTE YAMETOKANA NA USHIRIKIANO WANGU WA ZAMANI NA KAMPUNI YA SONY. LICHA YA KWAMBA TULISHAACHA KUFANYA KAZI PAMOJA KITAMBO, HADI LEO KAMPUNI HIYO BADO INASHIKILIA ZAIDI YA KAZI ZANGU 37, NA INAKATAA KUZIAACHIA. CHA KUSIKITISHA ZAIDI, SIPATI HATA SHILINGI MOJA KUTOKANA NA KAZI HIZO AMBAZO NI JASHO LANGU, JASHO LA MAISHA YANGU.
SERIKALI KUPITIA @cosotatanzania IMEJARIBU KUNISAIDIA NA KUSIMAMIA HAKI YANGU, LAKINI JUHUDI HIZO ZIMEKWAMISHWA KWA KUKOSA USHIRIKIANO KUTOKA KWA MWAKILISHI WAO, BI. SEVEN MOSHA. AMEKUWA AKIITWA MARA KADHAA BILA KUTOA USHIRIKIANO WOWOTE. HALI HII IMENIUMIZA SANA, IMENIVUNJA MOYO, NA INARUDISHA NYUMA NDOTO ZA WASANII WENGI AMBAO KIMYAKIMYA WANAENDELEA KUDHULUMIWA HAKI ZAO.
KWA UNYENYEKEVU MKUBWA, NAOMBA SERIKALI KUPITIA WAZIRI WETU, MHESHIMIWA PAUL CHRISTIAN MAKONDA (@BABAKEGAN), UINGILIE KATI SWALA HILI KWA HARAKA. NAOMBA HAKI ITENDEKE. NAOMBA JASHO LA MSANII LIHESHIMIWE. NAOMBA NDOTO ZETU ZISIZIDI KUKANDAMIZWA.
NIMECHOKA KUVUMILIA. NIMECHOKA KUNYAMAZA. NAOMBA HAKI.”
Suala hili linaendelea kuzua mjadala mpana miongoni mwa wadau wa sanaa na mashabiki, wakitaka kuona haki za wasanii zinalindwa kikamilifu katika enzi ya majukwaa ya kidijitali.

Hakuna maoni:
Chapisha Maoni