Breaking


Jumatano, 21 Januari 2026

TUHAKIKISHE KAMPASI MPYA ZA VYUO VIKUU ZINATOA MAFUNZO YA UJUZI

Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia imesisitiza kuwa vyuo vikuu vinavyojenga kampasi mpya katika maeneo mbalimbali nchini kuhakikisha kampasi hizo zinajikita katika kutoa mafunzo ya ujuzi (amali).  

Agizo hilo limetolewa jijini Dodoma na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda, wakati wa kikao kazi cha kimkakati kati ya wizara na wakuu wa taasisi zilizo chini ya wizara.  

Prof. Mkenda amesema kuwa hatua hiyo ni utekelezaji wa Sera ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 2014, toleo la 2023, inayosisitiza kuandaa wahitimu wenye ujuzi hivyo uwepo wa kampasi hizo ni fursa za kutoa mafunzo hayo na kusisitiza mafunzo kwa vitendo ili kujenga umahiri. 

Akizungumzia ufadhili wa masomo ya wanafunzi wa elimu ya juu, Prof. Mkenda amesema wizara inachukua hatua za makusudi kuhakikisha fursa zote za ufadhili wa masomo ya nje ya nchi zinatumika ipasavyo.  

"Kwa mfano kulikuwa na ufadhili wa masomo wa Saudi Arabia nafasi 127, lakini idadi ya wanafunzi walioomba na kunufaika nazo ni wachache. Tunahitaji kuangalia changamoto zinazokwamisha na kuzitatua," amesema Prof. Mkenda.  

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Mhe. Wanu Hafidh Ameir, amesema Wizara na Taasisi zinajipanga kimkakati kufikia malengo ya Taifa ya kuzalisha nguvu kazi yenye ujuzi utakao wezesha vijana kushiriki kikamilifu katika shughuli za uzalishaji na kuchangia maendeleo ya Taifa.  

Naye Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Carolyne Nombo, ameeleza kuwa kikao hicho cha kimkakati kimefanyika ili kuangalia utekelezaji wa Malengo ya mwaka 2025/26 na kuweka mikakati ya pamoja ya kufanikisha kwa malengo ya sekta na  Dira 2050.  


Ametaja baadhi ya mikakati iliyojadiliwa ni ile ya utekelezaji wa elimu ya lazima ya miaka kumi, uimarishaji wa mafunzo ya amali katika ngazi ya sekondari, pamoja na kuimarisha fursa za elimu ya juu na ufadhili.

Hakuna maoni: