Breaking


Jumamosi, 7 Machi 2026

MAWINGU NA MVUA KUTAWALA MAENEO MENGI NCHINI NDANI YA SAA 24 ZIJAZO



Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imetabiri kuwa katika saa 24 zijazo kuanzia saa 3:00 usiku wa Machi 7, 2026, maeneo mengi nchini yatakuwa na hali ya mawingu ikifuatana na mvua pamoja na ngurumo za radi katika baadhi ya maeneo. Mikoa ya Mtwara, Lindi, Morogoro, Tanga, Dar es Salaam pamoja na Mkoa wa Pwani ikiwemo visiwa vya Mafia, pamoja na visiwa vya Unguja na Pemba, inatarajiwa kuwa na mawingu mengi na vipindi vifupi vya jua huku mvua zikitarajiwa kunyesha katika maeneo kadhaa.


Kwa upande wa mikoa ya Dodoma, Singida, Arusha, Kilimanjaro na Manyara pamoja na mikoa ya nyanda za juu kusini ikiwemo Mbeya, Iringa, Njombe, Ruvuma, Rukwa na Songwe, hali ya mawingu inatarajiwa kuambatana na mvua na ngurumo katika maeneo machache pamoja na vipindi vya jua. Aidha, kwa mikoa ya Tabora, Kigoma, Katavi, Kagera, Geita, Mwanza, Shinyanga, Mara na Simiyu, hali ya hewa inatarajiwa kuwa na mawingu kiasi, mvua katika maeneo machache na vipindi vya jua.


TMA imetoa angalizo kuwa vipindi vifupi vya mvua kubwa vinaweza kujitokeza katika baadhi ya maeneo ya mikoa ya Arusha, Kilimanjaro, Manyara, Lindi, Mtwara, Tanga, Dar es Salaam, Morogoro na Pwani pamoja na visiwa vya Unguja na Pemba. Aidha, upepo wa pwani unatarajiwa kuvuma kutoka kaskazini mashariki kwa kasi ya takribani kilomita 30 kwa saa huku bahari ikitarajiwa kuwa na mawimbi makubwa kiasi. Mamlaka hiyo pia imeeleza kuwa hali ya mvua itaendelea katika maeneo mengi ya nchi hadi siku ya Jumatatu Machi 9, 2026.


Hakuna maoni: