Breaking


Jumanne, 28 Aprili 2026

MKUU WA WILAYA YA NJOMBE ATEMBELEA BANDA LA TASAC


Mkuu wa Wilaya ya Njombe mkoani Njombe, Mhe. Juma Sweda,  ametembelea Banda la Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC) na kupata elimu kuhusu shughuli mbalimbali zinazofanywa na TASAC ikiwemo kudhibiti na kusimamia usalama, ulinzi na utunzaji wa mazingira ya usafiri kwa njia ya  maji.

Akiwa Bandani hapo alifahamishwa kuhusu majukumu ya TASAC yakiwemo kudhibiti na kusimamia huduma za usafiri kwa njia ya maji, kudhibiti na kusimamia Usalama na ulinzi wa vyombo vya usafiri majini,  utunzaji wa mazingira na kutoa huduma ya Uwakala wa forodha kwa shehena mahsusi kwa mujibu wa sheria. 

Mhe. Sweda alifahamishwa kuwa shughuli zote hizi zinahusisha masuala  ya Usalama na Afya mahali pa kazi kwa ajili ya watumishi pamoja na wadau mbalimbali wanaopata huduma kutoka TASAC.

Kupitia ushiriki wake, TASAC inalenga kuongeza uelewa kwa wadau kuhusu umuhimu wa kuzingatia masharti na viwango vya usalama na afya kazini, hususan katika shughuli za usafiri majini. Elimu hiyo inasaidia kupunguza ajali na hatari zinazoweza kujitokeza, kulinda maisha ya watumishi na watumiaji wa huduma, pamoja na kuhifadhi mazingira ya maji.

Kwa upande wake, Mhe. Sweda amepongeza kazi zinayofanywa na TASAC, pia ameshukuru kwa kupata elimu hiyo.

TASAC inashiriki Maonesho ya Maadhimisho ya Wiki ya Usalama na Afya Mahali pa Kazi 2026 yanayofanyika Mkoani Njombe yaliyoanza tarehe 24 Aprili, 2026 na yanatarajiwa kufikia kilele  tarehe 30 Aprili, 2026 ambapo Kauli mbiu ya maonesho ya mwaka huu ni: “Mazingira bora ya Kisaikolojia na kijamii kazini ni njia ya kuimarisha ustawi wa wafanyakazi na kujenga taasisi imara.”

Hakuna maoni: