Breaking


Jumatano, 13 Mei 2026

KAFULILA: UBIA (PPP) NI NGUZO MUHIMU KATIKA KUIMARISHA SEKTA YA AFYA NA UUGUZI

Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi (PPP Centre), David Kafulila, amesema kuwa ubora wa rasilimali watu kupitia afya na elimu ndio msingi mkubwa wa Tanzania kufikia lengo la kuwa na uchumi wa dola trilioni moja ifikapo mwaka 2050.

Akizungumza kupitia mtandao wake wa kijamii wa X katika maadhimisho ya Siku ya Wauguzi Duniani, Kafulila alisema wauguzi ni mhimili muhimu wa sekta ya afya na maendeleo ya uchumi, kwani wao ndio waliopo mstari wa mbele kuokoa maisha ya wananchi.

“Uuguzi si kazi tu, bali ni wito wa kitume unaohitaji upendo, subira na utu wa hali ya juu. Wauguzi ni daraja kati ya wagonjwa na kupona,” alisema Kafulila.

Alieleza kuwa bila kuwa na jamii yenye afya bora, haiwezekani kuwa na nguvu kazi yenye tija, hivyo kufanya sekta ya afya kuwa msingi muhimu wa ukuaji wa uchumi mkubwa.

Kafulila alisema pamoja na juhudi kubwa zinazofanywa na Serikali katika kuboresha miundombinu ya afya, upatikanaji wa dawa, vifaa tiba pamoja na kuongeza wataalamu wa afya, bado Tanzania na Afrika kwa ujumla zinakabiliwa na changamoto ya upungufu wa wauguzi.

Kwa mujibu wa Shirika la Afya Duniani (WHO), uwiano unaopendekezwa ni wauguzi 45 kwa kila watu 10,000, huku Afrika ikiwa na wastani wa wauguzi 18 kwa watu 10,000. Katika nchi zilizoendelea, uwiano huo umefikia wauguzi 100 kwa watu 10,000. Alisema hali hiyo inaonesha wazi kuwa uwekezaji katika sekta ya afya, hususan uuguzi, unapaswa kuongezwa kwa kasi ili Tanzania iweze kufikia malengo yake ya maendeleo ya mwaka 2050.

Kafulila alisisitiza kuwa Serikali pekee haiwezi kubeba mzigo huo, hivyo mchango wa sekta binafsi ni muhimu katika kufanikisha uwekezaji wa afya na maendeleo ya taifa kwa ujumla. Alibainisha kuwa takwimu zinaonesha sekta binafsi inatarajiwa kuchangia asilimia 70 ya gharama za Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa kipindi cha mwaka 2026/27 hadi 2030/31, sawa na zaidi ya trilioni 334 za shilingi za Kitanzania.

Hakuna maoni: