Breaking


Ijumaa, 11 Septemba 2026

NGUVU YA MIKATABA YA USAFIRI WA ANGA KATIKA KUIUNGANISHA TANZANIA NA DUNIA

Mikataba ya Huduma za Anga baina ya Tanzania na nchi mbalimbali (BASA) inaendelea kudhihirisha umuhimu wake katika kuiunganisha Tanzania na mataifa mengine duniani. Mikataba hiyo huweka mfumo wa kisheria na kutoa haki za usafiri wa anga zinazowezesha mashirika ya ndege kuanzisha njia mpya na kupanua huduma za kimataifa, hivyo kuimarisha muunganiko wa Tanzania na masoko ya dunia. Hivi karibuni, mashirika ya ndege kama Brussels Airlines, Airlink, Etihad Airways, Neos na EgyptAir yameanzisha, kurejesha au kuongeza safari zake kupitia Dar es Salaam, Kilimanjaro na Zanzibar.


Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) ina jukumu muhimu katika kusaidia utekelezaji wa Mikataba hii kwa kusimamia haki za usafiri wa anga, kutoa idhini zinazohitajika na kuhakikisha kuwa mashirika ya ndege yanazingatia viwango vya usalama, kanuni na sheria zinazotumika. TCAA pia huipatia Serikali ushauri wa kitaalamu na kiufundi wakati wa majadiliano na utekelezaji wa mikataba hiyo, kwa lengo la kuongeza fursa za muunganiko wa anga.

Miongoni mwa safari/route mpya ni EgyptAir kuanzisha safari za moja kwa moja kati ya Cairo na Zanzibar kuanzia Septemba 2026. Aidha, Shirika la Ndege Tanzania (Air Tanzania Company Limited—ATCL) lilianza safari kati ya Dar es Salaam na Moscow, Urusi, mwezi Julai 2026. Hii inaonesha jinsi Mikataba hii inavyowezesha mashirika ya ndege ya Tanzania kukuza mitandao yake na kufikia masoko mapya ya kimataifa.


TCAA itaendelea kuishauri Wizara ya Uchukuzi na waendeshaji wa mashirika ya ndege kuhusu fursa zinazopatikana kupitia Mikataba kati ya Tanzania na nchi mbalimbali. Mikataba hii huyawezesha mashirika ya ndege yaliyoteuliwa kutoka Tanzania na nchi washirika kutoa huduma za usafiri wa anga kati ya nchi husika, kwa kuzingatia haki zilizokubaliwa na matakwa ya udhibiti. Hatua hii huchochea ongezeko la safari, utalii, biashara na uwekezaji.


Mikataba hii ni moja ya eneo linalochangia kuimarika kwa nafasi ya Tanzania katika usafiri wa anga wa kimataifa na kusaidia kufikiwa kwa malengo mapana ya kiuchumi na maendeleo ya nchi.

Hakuna maoni: