Breaking

Alhamisi, 18 Desemba 2025

WAZIRI KIJAJI ATAKA TAWA KUSIMAMIA IPASAVYO MIRADI 15 MPANGA KIPENGERE

Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji  ameitaka Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA) kusimamia vyema miradi 15 katika 

Pori la Akiba Mpanga Kipengere ili kuhakikisha inakamilika kwa wakati na jamii ianze kunufaika na matunda ya uhifadhi wa rasilimali za  Maliasili.

Mhe. Kijaji amesema hayo alipotembelea katika Pori hilo ikiwa ni mwendelezo wa kutembelea shughuli za Uhifadhi na vivutio vya Utalii vilivyopo hapa nchini, amesisitiza TAWA kutumia vyema fedha za serikali katika utekelezaji wa miradi hiyo kwa ubora na kiwango cha juu ikionesha uhalisia wa fedha zilizowekezwa.

"Hapa kuna miradi 15 iliyowekezwa katika kipindi hiki kifupi cha serikali ya awamu ya sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, niwatake TAWA kuweza kuisimamia kwa umakini miradi hii, iweze kudumu ili tuweze kufikia malengo yaliyokusudiwa ya uwepo wa miradi hii katika eneo letu, ili tuweze kuenzi kazi nzuri iliyofanywa na Rais wetu, ili thamani halisi ya fedha iweze kuonekana na wananchi waone matunda ya sh.billion 4.14 zilizowekezwa" amesema Mhe. Dkt.Kijaji

Aidha, Mhe. Kijaji ameilekeza Mamlaka hiyo kuangalia fursa mpya za  uwekezaji zilizopo kwenye  eneo hilo  na kuzitangaza ili kuendelea kuongeza  wageni kutoka ndani na nje ya nchi na hatimaye kufikia malengo ya serikali ya watalii Milioni 8 ifikapo mwaka 2030.

"Tuwaite wawekezaji, tuwauzie fursa wawekeze nasi li watanzania na wasio watanzania wanaofika hapa Mpanga Kipengere waweze kulala na  kula kwa amani kabisa, hivyo kaeni na mtoke na maandiko ya kuuza fursa tulizonazo kama alivyofungua mipaka Rais wetu kupitia Filamu ya Royal Tour" amesema Mhe. Kijaji.


Naye, Naibu Waziri wa Wizara hiyo Mhe. Hamad Hassan Chande , ametoa wito kwa Mamlaka hiyo kuendelea kuimarisha ushirikiano kati yao na jamii katika kulinda na kuhifadhi rasilimali za Taifa ili ziendelee kuwa na tija kwa kizazi hiki na kijacho ikiwa ni zao la asili 


"Endeleeni kuimarisha mahusiano yenu,  wanajamii mmekuwa walinzi wazuri wa rasilimali zetu. Niwasihi endeleeni  kuiishi vyema falsafa ya kazi na utu, hivyo niwaombe wanakijiji tuendelee kuhifadhi na kuzilinda  rasilimali zetu kwa wivu mkubwa sana kwa sababu hii ni neema aliyotupa Mwenyezi Mungu" amesema Mhe. Chande

 

Hakuna maoni: