Wanachama wa Shirika la Vyama vya watu wenye ulemavu Tanzania (SHIVYAWATA) Wilaya ya Mafia wameishukuru Tume ya Ulinzi wa Taarifa Binafsi (PDPC) kwa kuwapatia elimu kuhusu dhana ya ulinzi wa taarifa binafsi.
Hayo yamesemwa Machi 14, 2026 na mratibu wa mafunzo hayo yaliyofanyika katika ukumbi wa Lizu Mafia, Bw. Selemani Darusi ambapo amesema kundi la watu wenye ulemavu ni muhimu kupata mafunzo haya kwa wakati na ameishukuru PDPC kwa kukubali kuwaunga mkono.
“Tunaishukuru PDPC kwa kuitikia wito wa kutoa elimu kwa watu wenye ulemavu na ninawaomba wakati mwingine tukileta maombi ya uhitaji wa mafunzo msisite kutusaidia tena. Amesema Bw. Selemani Darusi
Kwa upande wa PDPC, Mkurugenzi wa PDPC ofisi ya Zanzibar, Bi. Rehema Abdala amewasilisha mada mbalimbali zikiwemo chimbuko la dhana ya Ulinzi wa Taarifa Binafsi, maana na aina za Taarifa Binafsi, uanzishwaji wa PDPC sambamba na majukumu yake, bila kusahau Ulinzi wa Taarifa Binafsi kwa watu wenye mahitaji maalum.
Ushiriki kwenye mafunzo haya ni sehemu ya PDPC kuhakikisha elimu ya Ulinzi wa Taarifa Binafsi inawafikia Wananchi wote nchini ili utekelezaji wa Sheria ya ulinzi wa Taarifa Binafsi uzingatiwe na hivyo kuwa na matokeo chanya katika Sekta ya Ulinzi wa Taarifa Binafsi nchini.



Hakuna maoni:
Chapisha Maoni