Breaking


Jumamosi, 21 Machi 2026

RAIS SAMIA AWATAKIA WATANZANIA EID AL-FITR NJEMA ASISITIZA UMOJA NA AMANI


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,  Dkt.Samia Suluhu Hassan, amewatakia Waislamu na Watanzania wote kwa ujumla sikukuu njema ya Eid al-Fitr, akisisitiza umuhimu wa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kufanikisha ibada ya Swaumu. Amesema ni vyema kuendelea kumuomba Mungu azipokee funga, dua na sadaka zilizotolewa katika Mwezi Mtukufu wa Ramadhani, huku akihimiza jamii kusherehekea sikukuu hiyo kwa furaha yenye mipaka ya maadili.


Aidha, Rais Samia ametoa wito kwa wananchi kuungana na ndugu, jamaa, majirani pamoja na marafiki katika kusherehekea kwa upendo na utulivu, huku wakidumisha mshikamano wa kitaifa. Ameeleza kuwa amani na umoja wa nchi ni msingi muhimu wa maendeleo, hivyo ni jukumu la kila Mtanzania kuilinda na kuithamini wakati wote.


Katika hatua nyingine, Rais Samia amesisitiza umuhimu wa kuyaendeleza mema yote yaliyojifunzwa wakati wa Ramadhani, ikiwa ni pamoja na upendo, huruma na kusaidiana. Ameongeza kuwa kuimarisha maadili mema katika jamii kutasaidia kujenga Taifa lenye mshikamano imara na lenye mwelekeo chanya wa maendeleo, akihitimisha kwa salamu ya “Eid Mubarak” kwa Watanzania wote.


Hakuna maoni: