Breaking


Jumanne, 17 Machi 2026

TPSF NA TPA WAJADILI TOZO ZA BANDARI 2026: SEKTA BINAFSI YAOMBA MAPITIO KWA UENDELEVU WA BIASHARA

Shirikisho la Sekta Binafsi Tanzania (TPSF), kwa kushirikiana na Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA), limeendesha mjadala wa ngazi ya juu wa sekta ya umma na binafsi (PPD – Public-Private Dialogue) uliolenga kujadili utekelezaji wa Ada za Bandari 2026 katika mazingira ya biashara

Mjadala huo uliwapa fursa wadau wa sekta binafsi kupata ufafanuzi wa kina kutoka TPA kuhusu dhamira, msingi, na umuhimu wa mabadiliko ya tozo zilizotangazwa tarehe 8 Machi 2026. Aidha, TPA iliwasilisha taarifa rasmi ikielezea mantiki ya marekebisho hayo pamoja na matarajio yake katika kuboresha ufanisi wa bandari na huduma za usafirishaji


Kwa ujumla, wadau wa sekta binafsi walionesha kuelewa dhamira ya serikali katika kuanzisha tozo hizo, hususan katika kuboresha miundombinu na ufanisi wa bandari. *Hata hivyo, walitoa maombi mahsusi ikiwemo kupunguzwa kwa kwa tozo pamoja na kuepuka utozwaji wa tozo hizo juu ya customs duty, wakieleza kuwa hali hiyo inaweza kuongeza gharama za biashara na kupunguza ushindani*

Akizungumza katika mjadala huo, Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa TPSF, Deogratius Massawe, alisisitiza kuwa shirikisho limepokea na kukusanya maoni ya wadau wake kwa umakini, na litaendelea kuyawasilisha kwa mamlaka husika ili kuhakikisha changamoto zinazojitokeza zinapatiwa ufumbuzi kwa wakati.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa TPA, Plasduce Mbossa, alieleza kuwa Serikali imekuwa sikivu kwa kupokea maoni kutoka kwa wadau mbalimbali, na akaihakikishia sekta binafsi kuwa *TPA si taasisi ya kuwazuia kufanya biashara, bali ni taasisi inayolenga kurahisisha na kuwezesha shughuli za biashara (facilitating institution)* .Aliongeza kuwa maoni yote yaliyotolewa yatafanyiwa kazi kwa kuzingatia maslahi mapana ya uchumi wa taifa.

Katika hitimisho la mjadala huo, wadau wote walikubaliana kuwa kuna umuhimu mkubwa wa kuongeza ufanisi wa bandari za Tanzania ili ziweze kushindana kikanda na kimataifa. Hata hivyo, walisisitiza kuwa mfumo wa tozo unapaswa kuwa stahimilivu kwa biashara (sustainable and business-friendly), na kwamba baadhi ya sekta au biashara zenye hali maalum (special cases) zinapaswa kupewa nafasi ya kuwasilisha athari zake kwa kina ili ziangaliwe kwa umakini zaidi na Serikali

Aidha, Serikali kupitia TPA ilitoa hakikisho kuwa itaendelea kushughulikia mapendekezo yote yaliyowasilishwa na wadau, na kwamba mrejesho rasmi utatolewa mara baada ya uchambuzi kukamilika kabla ya utekelezaji wa tozo kuanza tarehe 1/07/2026

Hakuna maoni: