Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran, Ismail Baghaei, amesema kwa sasa hakuna mpango wa kufanya duru ya pili ya mazungumzo na Marekani.
Akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari leo Jumatatu, alisema Marekani imeonyesha kutokuwa na uzito katika mchakato wa kidiplomasia, na kwamba imefanya vitendo vya uchokozi pamoja na kukiuka makubaliano ya kusitisha mapigano.
Baghaei aliongeza kuwa usafiri wa meli katika Mlango wa Hormuz hauwezi kurejea katika hali ya kawaida kwa upande mmoja pekee, kutokana na kile alichokiita “hali ya kivita” inayosababishwa na ukiukwaji wa makubaliano na vitisho vya Marekani dhidi ya bandari na meli za Iran.
Aidha, alisema Iran haiamini katika masharti ya muda au vitisho linapokuja suala la kulinda maslahi ya taifa, na kwamba kuondoa hifadhi ya nyuklia ya Iran si chaguo katika mazungumzo. Msisitizo wa Tehran ni kulinda mafanikio yake ya nyuklia ndani ya mipaka yake.
Alisisitiza pia kuwa Iran haina nia ya kuwa na uhasama na nchi za ukanda huo, akieleza kuwa hatua zilizochukuliwa katika siku 40 zilizopita zilikuwa ni “kujilinda kwa halali dhidi ya uchokozi wa kijeshi wa Marekani na Israel.”

Hakuna maoni:
Chapisha Maoni