Breaking


Jumamosi, 16 Mei 2026

SERIKALI YAPANGA MABORESHO YA MFUMO WA STAKABADHI GHALANI


                                    

Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Serikali inapanga kufanya maboresho katika mfumo wa stakabadhi ghalani ili kuondoa changamoto zinazowakabili wakulima hususan gharama na usumbufu wa kufuata huduma za maghala yaliyo mbali na maeneo yao ya uzalishaji.

Amesema hayo leo Jumamosi, Mei 16, 2026 wakati akizungumza na wananchi wa Kata ya Mnenia, Halmashauri ya Wilaya ya Kondoa mkoani Dodoma katika mwendelezo wa ziara yake ya kusikiliza na kutatua changamoto za wananchi.

Waziri Mkuu amesema Serikali imepokea malalamiko mbalimbali kuhusu utekelezaji wa mfumo huo na kwamba hatua zinaendelea kuchukuliwa ili kuhakikisha mfumo huo unawanufaisha wakulima kama ilivyokusudiwa.

Aidha, Waziri Mkuu amesema ataitisha kikao maalumu kitakachowahusisha wakuu wa mikoa pamoja na sekta zinazohusika kutoka maeneo yanayozalisha mazao yanayotumia mfumo wa stakabadhi ghalani ili kufanya tathmini ya changamoto zilizopo na namna ya kuzitatua.

Ametaja baadhi ya mikoa inayohusika kuwa ni Dodoma, Singida, Simiyu, Tabora pamoja na baadhi ya mikoa ya Kusini inayozalisha mazao ya biashara ikiwemo ufuta na dengu.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amesema Serikali imeelekeza wanunuzi wa mazao kutumia taasisi za kifedha kupata mikopo badala ya kuwakopesha wakulima kabla ya mauzo ya mazao yao.

Amesema Serikali itaendelea kufuatilia utekelezaji wa mfumo huo ili kuhakikisha wakulima wanapata huduma kwa urahisi na kunufaika ipasavyo na mazao yao.





Hakuna maoni: