Breaking


Jumatatu, 1 Juni 2026

KONGAMANO LA WANAMAWASILIANO WA SERIKALI 2026 LAANZA MWANZA

Kongamano la Wanamawasiliano wa Serikali 2026 limeanza rasmi katika Hoteli ya Malaika, jijini Mwanza, likiwakutanisha maofisa na wataalamu wa mawasiliano kutoka taasisi mbalimbali za Serikali nchini kwa lengo la kuimarisha utoaji wa taarifa kwa umma na kuendeleza mawasiliano yenye tija kwa maendeleo ya taifa.

Kongamano hilo linafanyika chini ya kaulimbiu isemayo “Taifa Moja, Sauti Moja, Simulizi za Dira 2050” (One Nation, One Voice, Communicating Vision 2050), ambayo inalenga kuhamasisha ushirikiano katika kuwasilisha na kufafanua kwa wananchi utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Katika kipindi cha kongamano hilo, washiriki wanatarajiwa kujadili masuala mbalimbali ya kimkakati yanayohusu mawasiliano ya Serikali, ikiwemo matumizi ya takwimu na ushahidi katika utoaji wa taarifa, mbinu za kukabiliana na taarifa potofu pamoja na njia za kuimarisha taswira ya Tanzania ndani na nje ya nchi.

Aidha, kongamano hilo linatoa jukwaa la kubadilishana uzoefu, kujifunza mbinu mpya za mawasiliano na kuimarisha ushirikiano miongoni mwa wataalamu wa mawasiliano wa Serikali ili kuhakikisha wananchi wanapata taarifa sahihi, kwa wakati na kwa ufanisi.

Kongamano la Wanamawasiliano wa Serikali 2026 limeandaliwa na Chama cha Maofisa Mawasiliano Serikalini (TAGCO) na linaendelea kufanyika jijini Mwanza kwa ushiriki wa wadau mbalimbali wa sekta ya mawasiliano na habari.



Hakuna maoni: