Breaking


Ijumaa, 5 Juni 2026

MADIWANI WA TEMEKE WATEMBELEA BANDARI YA DAR ES SALAAM KUJIFUNZA UENDESHAJI WAKE

Madiwani wa Halmashauri ya Manispaa ya Temeke wakiongozwa na Mstahiki Meya wa Manispaa hiyo, Mhe. Uzairu Abdul Athumani, wametembelea Bandari ya Dar es Salaam kwa lengo la kujionea shughuli mbalimbali zinazotekelezwa bandarini pamoja na kujenga uelewa wa pamoja kuhusu mchango wa bandari katika maendeleo ya uchumi wa taifa.


Ziara hiyo iliyofanyika Juni 4, 2025, imelenga kuwapa madiwani nafasi ya kufahamu kwa undani mifumo ya uendeshaji wa bandari, huduma zinazotolewa, pamoja na maboresho yanayoendelea kufanywa ili kuongeza ufanisi katika usafirishaji na biashara.


Akizungumza wakati wa mapokezi ya wageni hao, Mkurugenzi wa Bandari ya Dar es Salaam, Bw. Abed Gallus Abed, aliyemwakilisha Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA), Bw. Plasduce Mkeli Mbossa, alisema TPA inaendelea kutekeleza mikakati mbalimbali ya kuboresha huduma za bandari ili kuongeza ushindani na kuchochea ukuaji wa uchumi.


Kwa upande wao, madiwani wa Manispaa ya Temeke walieleza kuwa ziara hiyo imewapa uelewa mpana kuhusu shughuli za bandari na mchango wake katika kukuza biashara, uwekezaji na ajira kwa wananchi wa Tanzania.


Bandari ya Dar es Salaam ni lango muhimu la biashara kwa Tanzania na nchi jirani, ambapo inaendelea kuboreshwa ili kukidhi mahitaji ya sasa na ya baadaye ya usafirishaji wa mizigo katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kati.


Hakuna maoni: