Rais wa Marekani, Donald Trump, ameanza rasmi kutekeleza ushuru mpya wa kimataifa wa asilimia 10, kufuatia uamuzi wa Mahakama ya Juu ya Marekani kuzuia ushuru mkubwa wa uagizaji bidhaa uliokuwa umepangwa kuanza Ijumaa iliyopita.
Saa chache baada ya uamuzi huo, Trump alisaini amri ya serikali kuruhusu ushuru huo mpya kuanza kutumika kuanzia Februari 24. Hata hivyo, baadaye alitishia kuongeza kiwango hicho hadi asilimia 15, ingawa hadi sasa hajatoa agizo rasmi la kuongeza ushuru huo. White House haijatoa maoni rasmi kuhusu hatua hiyo licha ya mawasiliano kutoka vyombo vya habari.
Utawala wa Trump unatekeleza ushuru huo chini ya Kifungu cha 122 cha Sheria ya Biashara ya mwaka 1974, ambacho kinampa rais mamlaka ya kutoza ushuru kwa muda wa siku 150 bila kuhitaji idhini ya Bunge.
Akizungumzia hatua hiyo, mchambuzi wa masuala ya uchumi wa benki ya uwekezaji ING, Carsten Brzeski, amesema mabadiliko ya mara kwa mara ya sera za ushuru yanaongeza hali ya sintofahamu katika biashara ya kimataifa. Akizungumza na kipindi cha BBC Today, Brzeski alionya kuwa kuna hatari kubwa ya washirika wa kibiashara wa Marekani kuchukua hatua za kulipiza kisasi.
Kwa mujibu wa mchambuzi huyo, uwezekano wa kuzuka kwa vita kamili vya kibiashara sasa uko juu zaidi ikilinganishwa na mwaka uliopita, hali inayoweza kuathiri uchumi wa dunia na mnyororo wa biashara kimataifa.

Hakuna maoni:
Chapisha Maoni