Breaking


Jumanne, 21 Aprili 2026

“MAMA NTILIE SASA RASMI WATAITWA MAMA NA BABA LISHE” - RAIS SAMIA

 

Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania DKT Samia Suluhu Hassan amesema ni wakati sasa kwa jamii na taasisi za umma kuwatambua na kuwaheshimu wafanyabiashara wa chakula wadogo kwa hadhi sawa na sekta nyingine za uchumi, akisisitiza kuwa jina la “mama ntilie” libadilishwe na kuwa “mama na baba lishe” ili kuongeza heshima na thamani ya kazi hiyo. 

Amesema kundi hilo lina mchango mkubwa katika ajira na lishe kwa wananchi, hasa ikizingatiwa kuwa sekta isiyo rasmi inachukua takriban asilimia 70 hadi 80 ya ajira nchini, huku mamilioni ya Watanzania wakitegemea shughuli kama hizi kujipatia kipato.

Akizungumza jijini Dar es Salaam wakati wa ufunguzi wa kongamano la kitaifa la mama na baba lishe, Rais Samia amesema mabadiliko hayo yana lengo la kuondoa dhana potofu na kutambua mchango halisi wa sekta hiyo ambayo pia hutoa ajira kwa zaidi ya watu milioni 25 nchini. 

Ameongeza kuwa serikali itaendelea kuboresha mazingira ya biashara kupitia sera rafiki, miundombinu bora na upatikanaji wa mikopo, huku tafiti zikionyesha kuwa wafanyabiashara hao wanaweza kuingiza wastani wa zaidi ya shilingi laki nne kwa mwezi, kiasi kinachosaidia kuendesha maisha ya familia nyingi mijini na vijijini.

Aidha, Rais Samia ametoa wito kwa wadau kushirikiana na serikali kuwawezesha mama na baba lishe kwa mafunzo ya lishe bora, usafi na ujasiriamali ili kuboresha huduma wanazotoa kwa jamii. 

Licha ya mchango wao mkubwa, bado sekta hiyo inakabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwemo ukosefu wa leseni rasmi kwa baadhi ya wafanyabiashara na uhitaji wa kuimarisha viwango vya usafi. 

Amesema hatua za kuwaendeleza zitasaidia kuinua kipato chao na wakati huohuo kuboresha afya ya jamii kupitia upatikanaji wa chakula salama na chenye ubora.

Hakuna maoni: