Waandaaji wa mgomo huo wamesema kupanda kwa gharama za mafuta kumeendelea kuongeza ugumu wa maisha kwa wananchi wa kawaida huku sekta ya usafiri ikitajwa kuathirika zaidi. Aidha, wameitaka mamlaka ya udhibiti wa nishati na mafuta ya nchini humo, Energy and Petroleum Regulatory Authority (EPRA), kuvunjwa wakidai imeshindwa kudhibiti bei ya mafuta.
Mbali na usafiri wa abiria, mgomo huo pia unatarajiwa kuathiri shughuli za usafirishaji wa mizigo pamoja na sekta ya utalii katika maeneo mbalimbali ya Kenya kutokana na kupungua kwa huduma za usafiri.
Mgomo huo umeanza siku chache baada ya wahudumu wa usafiri wa umma kutangaza kuongeza nauli kwa asilimia 50 kufuatia kupanda kwa bei mpya za mafuta zilizotangazwa Mei 14, 2026.
Kwa mujibu wa bei hizo mpya, lita moja ya petroli katika jiji la Nairobi inauzwa kwa shilingi 214.25 huku dizeli ikiuzwa kwa shilingi 242.92, hali inayozidi kuongeza mzigo wa gharama kwa wananchi na wafanyabiashara.

Hakuna maoni:
Chapisha Maoni