Breaking


Jumamosi, 9 Mei 2026

WANAWAKE WAHIMIZWA KUTUMIA FURSA ZA KIUCHUMI KUJIKWAMUA KIMAENDELEO


Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Angellah Jasmine Mbelwa Kairuki, amewahimiza wanawake nchini kutumia kikamilifu fursa mbalimbali za kiuchumi zinazotolewa kupitia mikopo, uwekezaji, elimu ya fedha pamoja na manunuzi ya umma ili kujikwamua kiuchumi na kuchangia maendeleo ya Taifa.

Akizungumza katika hafla ya Mama Business Gala iliyofanyika jijini Dar es Salaam, Waziri Kairuki amesema wanawake wana nafasi kubwa ya kuleta mabadiliko chanya katika jamii endapo watatumia vyema fursa zilizopo katika sekta mbalimbali za uchumi na teknolojia.

Amesema ushirikiano miongoni mwa wanawake, uwekezaji katika elimu, afya na biashara ni muhimu katika kujenga jamii yenye maendeleo endelevu. Pia amewataka wanawake kuongeza matumizi ya teknolojia na majukwaa ya kidijitali ili kukuza biashara zao na kuongeza kipato.


Katika hotuba yake, Waziri Kairuki alisisitiza umuhimu wa malezi bora kwa watoto pamoja na matumizi sahihi ya mitandao ya kijamii na teknolojia, akieleza kuwa wanawake wana mchango mkubwa katika kulinda maadili na ustawi wa familia.


Aidha, amewataka wanawake kuendelea kuwa nguzo muhimu ya maendeleo ya kijamii na kiuchumi kwa kushiriki kikamilifu katika shughuli za uzalishaji, ubunifu na uongozi katika jamii.


Hakuna maoni: