Akizungumza na waandishi wa habari leo, Kaimu Meneja wa Mawasiliano na Uhusiano kwa Umma wa NEMC, Bi. Martha Kawishe, amesema wananchi wanapaswa kuendelea kulinda mazingira katika kipindi hiki ambacho mvua zinatarajiwa, huku wakiepuka shughuli zinazoweza kuongeza hatari ya mafuriko.
Kawishe amesema NEMC imewataka wananchi kutotupa taka kwenye mifereji, mito na makorongo, huku Mamlaka za Serikali za Mitaa zikisisitizwa kuhakikisha njia za maji zinasafishwa na kubaki wazi ili kurahisisha mtiririko wa maji.
Aidha, NEMC imesisitiza umuhimu wa kulinda kingo za mito, mabonde na maeneo oevu, pamoja na kuchukua hatua za kuzuia mmomonyoko wa udongo ambao unaweza kuongeza athari za mvua kubwa.
Baraza limesema litaendelea kushirikiana na Serikali za Mitaa pamoja na taasisi nyingine katika kutoa elimu kwa wananchi, kufanya ufuatiliaji na ukaguzi wa mazingira, pamoja na kuchukua hatua kwa mujibu wa sheria dhidi ya shughuli zinazoharibu mazingira.
NEMC imewahimiza Watanzania kufuatilia taarifa rasmi zinazotolewa na TMA na kuchukua hatua za tahadhari mapema. Baraza limesisitiza kuwa utunzaji wa mazingira ni hatua muhimu katika kupunguza athari zinazoweza kusababishwa na mvua kubwa na mafuriko.



Hakuna maoni:
Chapisha Maoni